Habari
WAZIRI NAPE ATAKA HUDUMA ZA MAWASILIANO ZIWE ZENYE TIJA NA KUBADILI MAISHA YA WATU

Na Jumaa Wange,WHMTH, ZANZIBAR
Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye (Mb) ametaka huduma za mawasiliano zinazotolewa kwa jamii kuwa zenye kuleta matokeo chanya na kubadi maisha ya watu.
Waziri Nape ameyasema hayo wakati akifunga Kongamano la Connect 2 Connect (C2C) lililofanyika katika ukumbi wa hoteli ya Madinat al Bahr, Zanzibar, Septemba 07, 2023.
“Tunataka tuondoke kwenye kuweza kumuunganisha mtu na huduma za mawasiliano tu, na kufanya huduma hizo ziwe na matokeo chanya kwenye maisha ya watu”. Amesema Waziri Nape.
“Na kumuunganisha mtu na huduma za mawasiliano kokote alipo liwe suala lenye kuleta tija na lazima huduma hizo ziwe zinapatikana, ziwe na ubora, ziaminiwe na zinapotumika ziwe na matokeo kwenye maisha yao katika maeneo mbalimbali yakiwemo Afya, kilimo na biashara”. Amesema Waziri Nape.
Pia Mhe. Nape ameipongeza kampuni ya Extensia Limited kwa kuandaa Kongamano hilo kubwa lililokutanisha wadau mbalimbali wa TEHAMA kutoka barani Afrika.